Sunday 20 November 2016

SOKO LA PILIPILI MBUZI




Na Hawa Mohamed na Tulinkisa Ndelwa  

      
Kijiji cha Luganga katika Halmashauri ya Wilaya ya Iringa Vijijini kina wakulima wengi wa pilipili, Wakulima hao wanakabiliwa na changamoto kadhaa katika kuwa na soko la uhakika la zao la pilipili mbuzi. 

Changamoto moja inatokana na ulimbukeni wa kukurupuka kulima pilipili kwa wingi kwa kutarajia kuwa bei nzuri ya msimu uliopita ndiyo itakuwa bei ya msimu unaofuata. Wakulima hao wamejikuta wakiingia katika mkumbo wa kuchangamkia kilimo cha pilipili mbuzi kutokana na msimu mzuri uliopita.Wakulima wengi hubabaika na hulima wakiangalia zao lenye bei nzuri na pindi bei inapoporomoka na kuwatia hasara wakulima hao huamua kuachana na pilipili mbuzi kabisa.

Mbali na hasara inayoweza kumkuta mkulima kwa kulima kwa wingi kwa matarajio ya bei kubwa na hivyo kuchangia mavuno kufurika na kuharibu bei, wakulima pia hukabiliwa na kutofahamu yaliko masoko ya bidhaa yao na hivyo kulazimika kutegemea wafanyabiashara wa kati – madalali. Madalali hao hununua pilipili mbuzi kwa bei ndogo kutoka kwa wakulima na kisha kuiuza kwa wafanyabiashara wengine kwa bei kubwa.

Mkulima YOHANES JUMANNE katika kijiji cha luganga, aliongea na IBER akasema alijiikuta anashindwa kung'ang'ania bei ambayo ni kinyume na matakwa ya madalili. Aisema moja ya vitu vinavyomfanya akose nguvu ya kudai bei bora zaidi ni kwamba soko linakuwa limefurika kiasi cha kuwafanya wakulima wengine kuachana kabisa na kilimo cha pilipili mbuzi. Aliongezea na kusema ufumbuzi unaweza kuwa eneo ambalo linatambulika wazi kuwa ni soko la pilipili mbuzi.

Kuwepo kwa soko la kudumu ni kitu ambacho kinaweza kumsaidia mkulima kupata kipato zaidi. Bei ya mazao inakuwa ni yakueleweka kwa kuwa hakutakuwa na madalali, wakulima watapata fursa ya kujiendesha wenyewe pia inaongeza ujuzi na maarifa juu ya soko na biashara kutokana na uwepo wa wataalamu juu ya masoko.

FIKIRA KISSIMBA ni Katibu Tawala Msaidizi, Uchumi na Uzalishaji, mkoa wa Iringa. Yeye alisema wakulima wasioweza kupata wateja wa mazao yao kwa haraka wanapaswa kuwa na eneo ambako ndio pekee pauziwe mazao yao.


Mindombinu ya uzalishaji, usafirishaji, uhifadhi na usindikaji ni muhimu katika kuimarisha uhakika wa masoko ya mazao ya kilimo. Japo bado kuna changamoto ya uelewa mdogo kwa wakulima. Licha ya kuwepo vikundi mbalimbali vya wakulima, bado ni wakulima hawajajiunga kwenye vikundi hivyo huathiri utendaji wa wataalamu wa kilimo. Jambo hili pia huchangia kukosekana kwa taarifa muhimu ikiwemo namna ya kukabiliana na changamoto zinazowakumba wakulima. Lakini wakulima wanapojiunga katika vikundi huku kila mmoja akiwa na mawazo tofauti na mwenzake, hupelekea kushindwa kuafikiana. Kumbe, kama anavyoeleza Katibu Tawala Fikira Kissimba, vikundi vyenye maafikiano vinaweza kusaidiwa mbinu mbalimbali zinaoweza kukabiliana na kufurika kwa soko, ikiwa ni pamoja na usindikaji wa mavuno ya ziada.

Faida ya wakulima kuwa kwenye vikundi inakwenda mbali zaidi kuliko kuwapa nguvu kwenye soko. Kuwa pamoja kunaisaidia serikali au wadau wengine kuwafikia wakulima kwa urahisi ili kutoa usaidizi wa kitaalamu wa kuboresha zao lao.

Nae Afisa Kilimo kata ya Ilolo Mpya, BWANA PETER SHAYO, alisema serikali inaweza kuwa na usaidizi mzuri kwa wakulima iwapo watalima pamoja katika vikundi. Anasema hilo linaweza kusaidia hata kwenye upatikanaji wa madawa.

Matokeo ya piilipili  kufurika katika soko hupelekea kuingia kwa madalali ambao wanawanyonya wakulima kwa kuwabana kwenye bei ya shambani.

Nini kifanyike?
Kutengwa  maeneo mahususi kwa uuzaji na ununuaji wa pilipili kutawapa wakulima uhakika wa soko na kujikinga na madalali wanaowanyonya. Nguvu ya wakulima pia inaongezeka kwa kuwa kwenye vikundi na hivyo kutohitaji madalali, kwa kuwa pia wanaweza kusaidiwa mikopo, madawa na ushauri na wadau wasiowanyonya. Na pia wakulima kupatiwa ustadi wa kusindika mavuno ya ziada.

Mzigo wa kuboresha soko kwa zao lao hilo, kwa sehemu kubwa limo mikononi mwa wakulima wenyewe. Wawe na ushirikiano ili wawe na nguvu na pia waweze kupata usaidizi.

No comments:

Post a Comment